
Magazeti ya Alhamisi, Mei 12, yanaripoti kwa kina kuhusu ugawanyaji wa mamlaka katika muungano wa Kenya Kwanza huku kiongozi wa ANC Musalia Mudavadi akitarajiwa kuteuliwa kuwa katibu mkuu wa Baraza la Mawaziri endpo muungano huo utashinda urais.
Magazeti haya pia yamegusia mchakato wa kumsaka mgombea mwenza wa Raila Odinga.
- Daily Nation
Chapisho hili linaripoti kwamba Naibu Rais William Ruto na hasidi wake mkuu kisiasa Raila Odinga wako nguvu sawa katika umaarufu wao, zikiwa zimesalia siku 88 tu kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9.
Kura ya maoni iliyofanywa na Nation Media Group ilibainisha kuwa wagombea hao wakuu wa urais wanaungwa mkono kwa asilimia 42.

Utafiti huo ulithibitisha kuwa uchaguzi wa urais utakuwa wa mbio za farasi wawili kati ya Ruto, anayewania kupitia UDA na Raila kwa tiketi ya muungano wa Azimio la Umoja One Kenya.
Utafiti huo ulionyesha kuwa Ruto anaungwa mkono sana katika maeneo ya Kati na Bonde la Ufa, akiwa na asilimia 60 na 61 mtawalia.
Kura hiyo ya maoni ilionyesha kuwa 10% ya wapiga kura hawajaamua kuhusu mgombea wao wa urais wanaompenda huku 5% wakikataa kujibu. Jumla ya 15% ambao hawajaamua itakuwa muhimu kwa matokeo ya uchaguzi wa urais mara tu watakapofanya maamuzi.
Hata hivyo, kama ilivyoonyeshwa na kura zingine za maoni, huenda uchaguzi wa urais ukaelekea duru ya pili iwapo hakutakuwa na mabadiliko makubwa ambayo yatasukuma wagombeaji wawili wakuu zaidi ya alama 50 kupata ushindi katika duru ya kwanza.
- The Standard
Gazeti hili linaripoti kuwa mshukiwa mkuu wa mauaji ya mwanariadha wa kimataifa Agnes Tirop amenyimwa dhamana.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Eldoret, Reuben Nyakundi, alikataa ombi la Ibrahim Rotich akisema upande wa mashtaka uliibua sababu za msingi.
Kulingana na upande wa mashtaka, Rotich ana uwezekano wa kushawishi au kuvuruga ushahidi.
- The Star

Gazeti hili linaripoti kwamba tume ya uchaguzi inataka maafisa wasimamizi waruhusiwe kufungua masanduku ya kupigia kura “wanapogundua kwamba waliweka vifaa kimakosa kwenye sanduku la kura lililofungwa”.
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka, IEBC, inaliomba Bunge kubadilisha sheria ili kuruhusu afisa msimamizi kufungua tena masanduku ya kura baada ya kufungwa mwishoni mwa kuhesabu kura katika hali nadra.
Nyenzo zilizoingizwa kwa bahati mbaya hazijaainishwa kwenye Mswada. Pendekezo hilo limo katika mswada wa kurekebisha kanuni za Uchaguzi Mkuu za IEBC 2022 ambao bado haujapitishwa na Kamati ya Bunge ya Kitaifa kuhusu Sheria Zilizokasimiwa.
Pendekezo la hivi punde la IEBC ni miongoni mwa msururu wa mabadiliko mengine yenye utata na makubwa katika kudhibiti utumaji matokeo.
- People Daily
Gazeti hili linaripoti kuwa Wabunge watakaochaguliwa Agosti 9, wanatazamiwa kulipwa zaidi ya KSh 1 milioni kila mwezi iwapo mapendekezo ya wabunge wa sasa kwa Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC) yatapitishwa.
Wabunge hao, katika kikao kisicho rasmi kilichojulikana kwa jina ‘Kamukunji’, walishinikiza nyongeza ya mishahara na marupurupu ya nyongeza pamoja na kubakiza posho zao za kuhudhuria vikao vya Bunge.
Waliapa kutosalimisha posho yao ya kuhudhuria kikao ya KSh 5000, ambayo huwa wanalipwa kila wanapohudhuria vikao vya bunge.
- Taifa Leo

Gazeti hili linaripoti kuwa Ruto aliiomba mahakama kutupilia mbali kesi iliyowasilishwa na watu waliodai kuwa wapiganaji wa Mau Mau wakitaka aondolewe afisini, wakidai kuwa alisusia majukumu yake kama naibu rais.
Ruto alisema kesi hiyo haina msingi na inalenga tu kupotezea mahakama muda.

Collins Oluyali is a popular columnist who reviews the Kenyan dailies every morning in the Magazetini section, giving it a political angle with facts weaved in rich Kiswahili. Collo is also a strategist in the WKT team.