Real Madrid inaialika Manchester City ugani Santiago Bernabeu kwa mchuano mgumu wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya saa nne kamili, saa za Afrika ya Mashariki.
Ikumbukwe timu hizi mbili sio lele mama. Ni moto wa kuotea mbali. Mechi ya raundi ya kwanza ugani Etihad, Man City walirindima Real Madrid mabao 4-3 katika ngaramba iliyosheheni shinikizo pande zote. Ikabaki mechi ya “funga nifunge”.
Raundi ya pili vikosi vyote vimejinoa makali kuchuana tena. Madrid na City zote zinatumia mfumo wa 4-3-3, hii ina maana kutakuwepo na mabeki wanne, viungo wa kati watatu na washambulizi watatu mbele.
Muamuzi wa mechi ya leo atakuwa Daniele Orsato muitaliano. Kwa ukufunzi, wa upande wa Real Madrid kuna Carlo Ancelotti huku kikosi Cha Man City kikisukwa na Pep Guardiola.
Wachezaji wa kikosi cha kwanza cha Real Madrid ni kama wafuatao: T.Courtois,D.Carvajal, E.Militao, Nacho, F.Mendy, Luka Modric, Casemiro, T.Kroos, F.Valverde, Kareem Benzema, Vincius Junior.
Manchester City wataanza na Ederson, J.Cancelo, Reuben Dias, A.Laporte, O.Zinchenko, B.Silva, James Rodri, Kevin De Bruyne, Riyadh Mahrez, Gabriel Jesus na Phil Foden.
Ni mechi ya patashika nguo kuchanika. Dakika tisini ndio zitaamua nani mbabe. Je, ni nani atambwaga mwengine?
Discover the pulse of Western Kenya with WKT – your go-to digital media platform for real-time updates, rich perspectives, and powerful stories that matter.