Mzee mmoja kutoka katika kijiji cha Kajoro, Teso Kusini katika kaunti ya Busia amewaacha wengi vinywa wazi baada ya kununua jeneza analosema ni la tatu katika matayarisho ya mazishi yake atakapofariki.
Mzee huyo wa umri wa miaka 87 kwa jina Aloise Otieng’i amesema amechukua uamuzi huo kuelimisha jamii ya Wateso kuhusu kujiandaa mapema
Mzee Otieng’i, ambaye aliwahi kuwa diwani kati ya mwaka 1984 na 1989, amekuwa na mazoea ya kununua majeneza tofauti.
“Nataka kuelimisha Wateso kwa sababu wewe unaweza kaa njaa na hakuna mtu anaweza kukuletea chakula, unaweza tembea uchi na hakuna mtu atakuletea nguo ila mtu anapokufa analetewa suti, anachinjiwa ng’ombe wengi lakini huwezi vaa hiyo nguo ama kula nyama hiyo,” alitoa busara mzee huyo.
Mzee Otieng’i amenunua jeneza la tatu sasa kwa kuwa ‘kimtindo hayafanani’.
“La kwanza nilinunua 2009, la pili 2012 na hili la leo nimenunua Sh58,000 ambalo nimeundiwa tu hapa. La pili nilinunua Sh12,000,” alisema.
Kando na kununua majeneza hayo, mzee huyo anasema anataka kuchimba kaburi na kulijenga vizuri.
Wenyeji wa eneo hilo wameibua hisia mseto, wengine wakimuunga mkono na wengine wakisema ni kinyume na maandiko yaliyochapishwa ndani ya vitabu vitakatifu.
Tom Lutali is a seasoned scribe based in Lugari Sub-County in Kakamega County who writes human interest stories and sports for WKT.