Magazeti ya Alhamisi, Machi 30, yanaangazia kwa upana maandamano ya Azimio la Umoja dhidi ya serikali huku kukiwa na wito Rais William Ruto na Raila Odinga wakumbatie mazungumzo.
Daily Nation
Chapisho hili linaripoti kwamba kuna mgawanyiko katika utawala wa Ruto kuhusu namna ya kukabiliana na maandamano ya Azimio na uvamizi wa ardhi ya rais wa zamani Uhuru Kenyatta
Mvutano huo ni kati ya wale wanaotaka hatua za haraka na madhubuti zichukuliwe dhidi ya uvamizi katika shamba la Kenyatta huku wengine wakipinga na kuhoji kuwa rais huyo wa zamani hafai kuchukuliwa kuwa tofauti na Wakenya wengine ambao wamepoteza mali kwenye maandamano.
Inaarifiwa kuwa rais huyo wa zamani anataka kushughulikiwa suala hilo kisheria.
Kuhusu maandamano, inaripotiwa kuwa mgawanyiko uliibuka katika muungano wa Kenya Kwanza baada ya Waziri wa Usalama Kithure Kindiki kupinga wito wa maafisa wa usalama kutumia nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji na pia kupuuza malalamishi kuhusu maandamano ya Jumatatu.
Pia kuna madai kuwa kulikuwa na mpango wa kuzima mtandao wakati wa maandamano ya Jumatatu, lakini ukakatizwa na Ruto, ambaye alitilia shaka busara yake.
Huku hayo yakijiri, seneta wa Uasin Gishu Jackson Mandago ametoa onyo kali kwa Inspekta Mkuu wa Polisi Japhet Koome na kuahidi kuwa ataitwa Bungeni kuhojiwa na kuanzisha mswada wa kutimuliwa kwake kuhusiana na namna aliyoshughulikia maandamano ya Jumatatu.
Taifa Leo
Gazeti hili linaripoti kuwa mwanahabari wa zamani wa runinga, Jacque Maribe, na aliyekuwa mpenzi wake Joseph Irungu almaarufu Jowie wana kesi ya kujibu kuhusu mauaji ya mwanabiashara Monica Kimani aliyeuawa mwaka wa 2018.
Uamuzi huo ulitolewa Jumatano, Machi 29, na Jaji Grace Nzioka katika Mahakama Kuu ya Naivasha baada ya kutathmini ushahidi uliowasilishwa na upande wa mashtaka.
Monica Kimani alikumbana na mauti yake saa chache baada ya kurejea nchini akitokea Sudan Kusini mnamo Septemba mwaka wa 2018.
The Standard
Walimu wa shule za chekechea sasa wana kila sababu ya kutabasamu baada ya mahakama kusitisha mipango ya serikali ya kupunguza nusu ya mishahara yao ya kila mwezi.
Jaji Ann Mwaure aliamuru serikali kudumisha mishahara ya sasa hadi kesi iliyowasilishwa na mwenyekiti wa Chama cha Walimu wa Shule za Upili na Vyuo vya Kadri (KUPPET), Omboko Milemba, isikizwe na kuamuliwa.
Milemba aliishtaki Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC) baada ya kupendekeza mishahara yao kupitiwa upya.
Hatua hiyo iliathiri walimu 45,000 wa chekechea ambao walikuwa kwenye hatari ya mishahara yao kukatwa kwa 50%.
People Daily
Gazeti hili linaripoti kuwa mama yake aliyekuwa Gavana wa Kisii James Ongwae amemshtaki Gavana wa Siaya James Orengo kwa madai ya kumrushia cheche za matusi wakati wa mkutano wa Azimio mnamo Februari.
Grace Moraa alisema Orengo alimdunisha hadhi na kukiuka haki zake za kibinadamu alipomtusi akitumia maneno machafu na yaliyomharibia jina na kuzua kashfa ya uongo dhidi yake.
Collins Oluyali is a popular columnist who reviews the Kenyan dailies every morning in the Magazetini section, giving it a political angle with facts weaved in rich Kiswahili. Collo is also a strategist in the WKT team.